Tuesday, 15 March 2016

UTUKUFU NI MBELE KWA MBELE

Mungu alichokuwekea hakiozi. Ni methali ya Tanzania. Ni methali ambayo inatia matumaini kwa watafutaji na waliokata tamaa. Makubwa Mungu aliyokuwekea yatafunuliwa mbele kwa mbele. Utukufu ni mbele kwa mbele. Mungu anaweza kubadili miiba ikawa maua, anaweza kubadili hasi ikawa chanya, anaweza kubadili machozi ya huzuni yakawa machozi ya furaha. Katika nyufa za maisha Mungu anaweza kuleta mwanga wa matumaini. Mwandishi wa nyimbo  Leonard Cohen aliandika, “Kuna nyufa katika kila kitu; hivyo ndivyo mwanga unavyoingia.” Kioo cha mbele cha gari ni kikubwa kuonesha kuwa makubwa yako mbele. Vioo vya upandeni vya kutazama ya nyuma ni vidogo kuonesha kuwa madogo yako nyuma, utukufu ni mbele kwa mbele. Yesu alipogeuka sura mlimani alitaka kuwaonesha mitume wake utukufu ni mbele kwa mbele.
Mitume wa Yesu wamekata tamaa Yesu alipowaambia atasulubiwa msalabani. Katika maisha yao palikuwepo na ufa wa kukata tamaa. Yesu alipogeuka sura mlimani mwanga wa matumaini uliingia katika nyufa zao za kukata tamaa. Petro alimwambia Yesu, “Mwalimu, ni vizuri kwetu kukaa hapa; tutajenga vibanda vitatu, kimoja chako, kimoja cha Musa, na kimoja cha Eliya.” (Luka 9: 33).   Petro hakujua kuwa utukufu ni mbele kwa mbele. “Petro hakulielewa bado neno hilo alipotamani kuishi na Kristo mlimani. Amekuwekea hayo, Petro, baada ya kifo chako lakini sasa yeye mwenyewe anakuambia: shuka kuangaika duniani, ukatumikie duniani, ukadharauliwe, ukasulubiwe duniani.Uzima umeshuka ili kuuawa:Njia imeshuka ili isikie uchovu wa duniani; chemichemi imeshuka ili kupata kiu;nawe wakataa kuteseka? (Mt. Augustino Sermo 78,6: PL38,492-493;Lk9:33). Mtaka cha uvunguni sharti ainame. Utukufu utakaopatikana mbele kwa mbele lazima kuufanyia kazi.
Yesu alipowatibu wakoma kumi aliwaambia waende wajioneshe kwa makuani. Bila shaka kabla ya kuondoka walisema hatujapona aliwaambia nenda. Biblia inatwaambia walipokuwa wanaenda wakapona. Utukufu ni mbele kwa mbele. Nelson Mendela alipofungwa Roben Island miaka aliyokaa kwenye kisiwa hicho aliita miaka yenye giza. Lakini utukufu ni mbele kwa mbele baada ya kukaa gerezani miaka 27 alikuwa Rais wa Afrika ya Kusini. Baada ya miaka yenye giza alipata miaka yenye mwanga.
Watunzi wa hadithi na filamu hutumia mbinu inayoitwa “ploti” ambapo mhusika mkuu hupata matatizo makubwa na changamoto kubwa. Mwishowe hufanikiwa na hivyo kufanya hadithi au filamu ivutie. Mungu ni Mtunzi wa watunzi ni Muumba wa watunzi. Anapotengeneza hadithi ya maisha yetu anataka mwisho wa siku ivutie. Anaweza kukupitisha kwenye matatizo makubwa mwisho wa siku utukufu ni mbele kwa mbele. Yesu alipowaambia wafuasi wake kuwa atakufa msalabani jambo hilo lilisababisha wingu zito la kukata tamaa katika maisha ya mitume. Aligeuka sura kuwakumbusha mwisho wa mambo utakuwa huo. Petro aliposema kujenga vibanda vitatu bila kujua ulikuwa ni utabiri wa kujenga Kanisa. Yesu alisema: “Wewe ndiwe Petro na juu ya mwambao nitalijenga Kanisa langu wala milango ya kuzimu haitalishinda.” Baba wa Kanisa Damas alikuwa na haya ya kusema: “Lakini Bwana hakukufanya uwe mjenzi wa vibanda bali wa Kanisa la ulimwengu wote. Maneno yako yametimizwa na wafuasi wako, kondoo wako kwa kujenga kibanda, si kwa ajili ya Kristo tu, bali kwa ajili ya watumishi Wake. Lakini Petro hakusema hili kwa makusudi bali  kwa kupitia ufunuo wa Roho Mtakatifu akifunua mambo yatakayokuja.” Ukweli huu unabainisha umuhimu wa wazo letu, utukufu ni mbele kwa mbele.
“Sijui kikomo chako kitakuwa kipi, lakini neno moja najua: baadhi yenu watakaofurahi watakuwa wale ambao wametafuta na kugundua umuhimu wa namna ya kutumikia,” alisema Albert Schweitzer. Ili kupata furaha ya kugeuka sura ilibidi Petro na wenzake washuke chini ili kuufanyia kazi utukufu wa mbele kwa mbele. Mtoto anapopelekwa shule wazazi hawajui atakuwaje mbeleni utukufu ni mbele kwa mbele. Kuna mwalimu wa shule ya awali aliyekuwa anawainamia watoto wadogo walipokuwa wanaingia darasani. Alipoulizwa kwa nini alifanya hivyo alisema: “Hao watoto ni wabunge wa kesho, ni maprofesa wa kesho, ni wafanyabiashara wa kesho.” Ni kweli utukufu ni mbele kwa mbele.

No comments:

Post a Comment